Friday 6 February 2015

AFYA: MTOKI /TEZI /SWOLLEN LYMPH NODES(GLANDS)


Mtoki au kwa lugha ya kitaalamu, swollen lymph nodes or glands, ni uvimbe wa tezi unaojitokeza katika mwili wa mtu baada ya mwili kuumia na kushambuliwa na vijidudu au bakteria wasababishao magonjwa au wavurugao utendaji kazi wa kawaida wa mwili.

Tezi hizi (lymph nodes/glands) zinapatikana sehemu mbalimbali katika mwili, na kazi zake maalumu ni kugundua na kushambulia vitu au wadudu mbalimbali wanaoingia katika mwili na kusababisha magonjwa, hivyo ni kitu muhimu sana katika ulinzi au kinga ya mwili. Miongoni mwa sehemu katika mwili ambapo tezi hizi hupatikana ni maeneo ya nyonga (groin), nyuma za masikio, chini ya taya na kidevu, nyuma ya kichwa, maeneo ya kwapani (armpit) na shingoni.
Mara nyingi vitu vinavyosababisha mtu apate mtoki ni pamoja na mtu kupata maambukizi ya magonjwa mfano ugonjwa wa vidonda koo au tonsillitis, lakini mbali na maambukizi pia mtu anaweza kuwa kaumia sehemu ya mwili mfano mguuni kapata kidonda, ingawaje kupata mtoki SIYO lazima uwe na kidonda, mtu pia anaweza kupata mtoki kutokana na mambo ya kinga ya mwili kutokuwa katika hali nzuri, mfano endapo mtu ana ugonjwa kama vile ugonjwa wa joints za vidole vya mikononi na miguuni, Rheumatoid Arthritis, au endapo mtu ana upungufu wa kinga mwilini, UKIMWI, anaweza kupata mtoki, pamoja na hayo inawezekana mtu akawa na matatizo ya damu, kansa ya damu, leukemia, pia anaweza kupata mtoki.

Dalili za mtoki ni pamoja na maumivu sehemu yenye tezi, mfano inawezekana ikawa ni kwapani, katika nyonga au shingoni, mtu anaweza kupata homa, sehemu husika inaweza kuwa nyekundu (hii ni kutokana na kuongezeka kwa mtiririko wa damu katika sehemu hiyo).
Katika hali ya kawaida ni vigumu kuweza kuishika sehemu ya mwili na kuihisi tezi, hii ni kutokana na udogo wake, ina umbo la punje ya haragwe na ukubwa wake ni kitu kisichozidi inch moja. Endapo mtu kapata maambukizi au kaumia au kapata kitu chochote kile kinachoweza kuifanya tezi ivimbe, ndipo mtu utakapoweza kuishika sehemu husika na kuweza kuihisi tezi katika mwili wako.

Mtoki unaojitokeza ghafla na unakuwa na maumivu mara nyingi husababishwa na kuumia sehemu ya mwili au mwili kupata maambukizi fulani mfano vidonda kooni, tonsillitis.
Kutegemeana na historia ya mgonjwa au mtu mwenye uvimbe huu, daktari atapendekeza aina fulani ya vipimo vifanyike ili kuweza kutoa mwangaza wa tiba gani uweze kupewa. Kuna baadhi kama nilivyokwisha kueleza hapo awali kuwa chanzo inawezekana kikawa ni maambukizi ya vijidudu mfano bakteria, hivyo daktari atafanya maamuzi ni kundi lipi la dawa (antibiotics) litafaa kulingana na hali yako, pia kuna wengine wanao uvimbe ambao hauna maumivu na pengine ukubwa wake unaongezeka siku hadi siku, hapa pia inawezekana kikawa ni kitu kingine na baada ya vipimo vya kutosha huduma sahihi inaweza kutolewa.

Mpenzi msomaji, makala hii nimeiandika ili kukushirikisha mawazo kuhusu kile unachokifahamu kuhusu mtoki, na siyo njia mbadala ya kukufanya usifike katika wataalamu wa afya endapo utakuwa na tatizo hili, fika kwa wataalamu walio karibu nawe ili kuweza kujua namna bora zaidi ya kukusaidia.

Credit : Tanzalife

Thursday 5 February 2015

BOBBY KRISTINA MAHUTUTI KWA AJILI YA MADAWA YA KULEVYA

Ule usemi usemao maji hufuata mkondo unauhalisisa wake.
mtoto wa aliyekua Muimbaji Maarufu dunian Marehemu Whitney Houston naye aangukia katika janga la madawa ya kulevya na kusababisha hali yake kua mbaya baada ya kukutwa amezimia ndani ya Jacuz baada ya kulewa na madawa.

katika mazingira hayo alokutwa Bobbi Kristina akiwa amezimia ndani ya maji na kuwahishwa hospital kwa ajili ya uchunguzi na matibabu, ni sawa na mazingira ambayo alikutwa mama yake Whitney Houston akiwa tayari ameshafariki huku akiwa ameinamisha kichwa kwenye maji.

Kwa tukio la juzi, tovuti ya CNN iliarifu kuwa binti huyo wa mwanamuziki Bobby Brown alifikwa na hali hiyo mwishoni mwa wiki huku ndugu yake wa karibu akimweleza mwandishi wa tovuti hiyo, Sunny Hostin kwamba baada ya kugonga mlango mara kadhaa bila majibu, alipata shaka na kuingia ndani na kumkuta Bobby katika hali hiyo na kupiga simu polisi, ambao walifika na kumkuta akiwa na hali mbaya kisha kumpeleka katika Hospitali ya North Fulton.
Msemaji wa Polisi, Lisa Holland aliiambia tovuti hiyo kuwa walipofika walimkuta Bobby hapumui, lakini baada ya kufikishwa hospitali na kupatiwa huduma ya kwanza alianza kupumua, ingawa alikuwa hajitambui.
Tovuti ya TMZ imeripoti kuwa baada ya Polisi kufanya ukaguzi walikuta dawa za kulevya.
Kwa mujibu wa TMZ, siku moja kabla ya tukio Bobbi Kristina alikuwa na rafiki yake Maxwell Byron Lomas, ambaye mwezi mmoja uliopita alikamatwa kwa kusambaza dawa za kulevya na kuwekwa chini ya ulinzi na baadaye aliachiwa kwa dhamana.
Taarifa kutoka Polisi zinazoandikwa katika jarida la Fulton County Jail records zinasema Lomas amekuwa akihusishwa na kashfa ya dawa za kulevya kwa muda mrefu na siku moja kabla ya tukio hilo alikuwa na Kristina pamoja na mumewe Gordon.
Ilivyokuwa kifo cha Whitney
Whitney Huston alifariki dunia Februari 11, 2012 katika Hoteli ya Beverly Hilton jijini Los Angeles, saa chache kabla ya kufanya onyesho kwenye sherehe za maandalizi ya Tuzo za Grammy.
Mkuu wa Polisi wa Beverly Hills, Luteni Mark Rosen alithibitisha kukutwa kwa aina fulani ya vidonge vya kutuliza maumivu katika chumba alichofia mwanamuziki huyo, huku kukiwa na ushahidi kuwa alikuwa akitumia dawa za kulevya baada ya kushindwa kutumbuiza jukwaani mara kadhaa na kukaa kimya ‘akisikilizia’ kama wafanyavyo mateja.
Whitney ambaye alikuwa gumzo miaka ya 1980 na 1990 kutokana na sauti yake ya kumtoa nyoka pangoni na baadaye kwenye ushiriki wake katika filamu za ‘The Body Guard’ na ‘Waiting to Exhale’ aliwahi kukaririwa akisema baada ya kuanza kuyumba kwa afya yake: “Nina shetani mkubwa ananiandama, kama siyo marafiki zangu, basi ni maadui zangu au ni akili yangu inayonituma kufanya vitu ambavyo vitagharimu maisha yangu.”.



Wednesday 4 February 2015

TEVEZ AFUNGUKA KUHUSIANA NA MATESO ALOYAPATA .


Kile kisa cha mtalaka wa mwimba taarab mahiri Bongo, Aisha Ramadhani Nkongo ‘Isha Mashauzi’, Jumanne Hassan ‘Tevez’ kuteswa na kudhalilishwa nchini Afrika Kusini kisa kikidaiwa ni kudhulumu mzigo wa wafanyabiashara wenzake kimeingia awamu nyingine!
Kwa mara ya kwanza Gazeti Pendwa la Amani Tanzania limeweza kuzungumza na Tevez kwa dakika arobaini na tano kutokea nchini humo ambako anauguza majeraha.


KWANZA SIKU YA TUKIO
Kabla Tevez hajasimulia kilichompata na hali yake kwa sasa, ni muhimu kukumbuka kuwa, tukio hilo ambalo lilikuwa habari ya Jiji la Dar es Salaam, lilijiri mwishoni mwa wiki iliyopita ambapo picha zake zilizagaa zikimuonesha akiwa amefungwa kamba huku mwili wake ukiwa umetapakaa damu na majeraha kadhaa.

AMANI LAMSAKA
Kwa vile habari za tukio hilo ziliandikwa na baadhi ya vyombo vya habari bila kupata balansi (uwiano) na Tevez mwenyewe, Amani liliingia kazini kumsaka mhanga huyo usiku na mchana.

MSIKIE SASA
Akizungumza kwa hisia kali na gazeti hili juzi, Februari 3, mwaka huu kutoka Mji wa Durban, Afrika Kusini, Tevez alisema:
“Kusema ukweli tukio lililonikuta watu huko nyumbani (Bongo) wanalitafsiri tofauti sana. Nimesikia kwamba wanasema eti nilidhulumu mzigo wa mtu, ndiyo maana niliteswa! Si kweli.”


UKWELI NI UPI?
“Ishu iko hivi, mwenyeji wangu hapa Durban, anaitwa Ibra, ndiye ambaye alinipokea siku nilipotua hapa.
“Huyu bwana inaonekana  ni tamaa. Aliniundia njama, aliita wenzake na kuniteka kisha kunitesa sana wakidhani nina pesa nyingi.
“Niliteswa sana kwa kweli. Kama mlivyoona picha. Nilidhalilishwa sana, lakini katika yote ukweli sijadhulumu mzigo wa mtu.”

ULICHOPOTEZA KATIKA UTESWAJI
 “Katika mateso yangu, walifanikiwa kunipora Dola za Marekani elfu 14 (kama shilingi milioni 22) na Landi za Afrika Kusini elfu 3 (shilingi 480,000) zikiwemo simu zangu mbili aina ya Sumsung na Nokia ambayo nilikuwa naitumia sana kuwasiliana na watu wangu muhimu.”

HAIKUWA KAZI RAHISI
Tevez akazungumzia jinsi jamaa walivyomkamata: “Jamaa siku wananiteka usiku kiukweli nilipambana nao sana hadi wanafikia hatua ya kunizidi nguvu na kunifunga kamba. Nilikuwa nimewachapa kwelikweli ila kwa vile walikuwa wengi na walikuwa wakitumia silaha nilijikuta nikiishiwa nguvu baada ya kunipiga na kitu kizito kichwani nikapoteza fahamu, nilipojitambua ndiyo nikakuta wamenifunga kamba.”

KINACHOKUUMA NINI?
“Tukio linaloniuma zaidi ni yule jamaa ambaye anaonekana katika picha amekaa jirani na mimi, hana shati. Alinichoma pasi mgongoni, namchukia sana lakini nimemwachia Mungu.”

KUHUSU KUKATWA NYETI, KUFANYIWA KITU MBAYA
Tevez: “Nasikia watu huko Tanzania wanazusha eti nimekatwa nyeti, si kweli kabisa. Mimi nimepigwa na kuchomwa pasi wala hakuna kitu kama hicho zaidi ya kunichoma na pasi.
“Nimesikia wengine wanasema nimetobolewa macho, huo ni uzushi wa watu tu! Mimi niko safi na hali yangu ya kiafya inaendelea vizuri.”

SABA WAMEKAMATWA
Tevez tena: “Nashukuru sana serikali ya huku wameweza kunisaidia kwani mpaka sasa ninapoongea na wewe Musa Mateja hawa jamaa wamekamatwa saba.
“Jana (Jumatatu) walifikishwa mahakamani na kusomewa mashitaka ya kunishambulia na kupora fedha. Wanatarajiwa kurejea tena mahakamani baada ya siku 7, ingawa nimeambiwa kesho (jana Jumatano) wataletwa Polisi Central ya huku kwa ajili ya mimi kuwatambua zaidi.”

BONGO LINI TEVEZ?
“Bongo natarajia kurudi Alhamisi (leo) au Ijumaa (kesho) kama mambo yangu yatakuwa kwenye mstari ila pia sasa hivi natarajia kuwasiliana na balozi wetu ili nijue kama ana taarifa zangu na namna ambavyo ataweza kunisaidia kama kiongozi wangu.”

HALI YAKO KWA SASA
“Kusema ukweli naendelea vizuri ni majeraha tu ambayo hata hivyo yanakauka. Ila hili la pasi mgongoni ndiyo  linasumbua kwa mbali, lakini naamini litakaa sawasawa.”

Na Mussa Mateja.